Enter Adress

Tuesday, October 30, 2012




Mwenyekiti wa Kamati ya Miss Tanzania, Bw. Prashant Patel (katikati) akizungumza wakati wa uzinduzi wa tovuti itakayokuwa inajulikana kama www.misstanzaniatreasures.com mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam.  Wengine katika picha ni Mkurugenzi Mtendaji wa tovuti hiyo, Bw. Ali Zoeb (kushoto) na mshauri wa habari wa tovuti hiyo, Bw. Peter Keasi.

MISS TANZANIA YAZINDUA TOVUTI YASISITIZA UMUHIMU WA UREMBO



Jamii imesisitizwa kuona shughuli za urembo kama fani nyingine ambayo ikifanywa vizuri inaweza kumkomboa mshiriki kiuchumi na kumuibua kama mtu wa muhimu katika jamii.

Wito huu umetolewa na Mwenyekiti wa Kamati ya Miss Tanzania, Bw. Prashant Patel aliyekua mgeni rasmi katika uzinduzi wa tovuti ya mashindano hayo, www.misstanzaniatreasures.com, mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam.
“Lengo la tovuti hii ni kutaka kueneza elimu hiyo na kuonyesha kwamba urembo ni kazi au fani kama nyingine na wala haina uhusiano wowote na uhuni kama baadhi ya watu wanavyoendelea kuamini,” alisema Bw. Prashant.
Alisema wengi wa warembo waliowahi kufanikiwa kutwaa taji la Miss Tanzania leo hii ni watu wenye mafanikio makubwa, kila mtu akifanya kile anachokipenda na kukiweza. 
Alisema tovuti hiyo inataka kuwaibua siyo tu washindi wa Miss Tanzania waliopita, bali washiriki mbalimbali waliwahi kushiriki katika mashindano hayo na kuonyesha wako wapi, wanafanya nini, ndoto na matarajio waliyonayo na hata changamoto wanazokumbana nazo.
Hadi sasa kuna jumla ya washiriki zaidi ya elfu tano tangu Miss Tanzania ianzishwe mwaka 1994. 
Alisema kamati ya MissTanzania inaamini warembo hawa ni hazina na hivyo wanataka kuonyesha hazina iliyopo katika taifa.
Alisema juhudi hizi za kuanzishwa kwa tovuti hii zitafuatiwa na uanzishwaji wa jarida litakalojulikana pia kama Miss Tanzania Treasures.
Akielezea zaidi alisema sehemu ya faida itakayotokana na tovuti hii na jarida hilo itatumika katika kuchangia maendeleo ya warembo hawa kama elimu na shughuli mbalimbali wanazofanya kwa utaratibu utakaopangwa.  Pia, faida itakayopatikana itatumika katika kusaidia watoto yatima hapa nchini.
“Tovuti hii itasaidia dunia nzima kushuhudia na kujua kwa undani kuhusu Miss Tanzania.  Hii ni fursa nyingine katika kukuza sekta ya utalii hapa nchini maana hakuna ubishi kwamba Miss Tanzania imekua moja ya njia za kukuza utalii wetu nje ya nchi,” alisisitiza.
Akielezea zaidi alisema tovuti ni njia muafaka katika kipindi hiki cha Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ambapo maendeleo yanategemea zaidi ufanisi katika mawasiliano.
“Tovuti hii itasaidia kujenga mtandao baina ya warembo wenyewe na wakajua jinsi ya kushirikiana katika maswala mbalimbali ya kijamii na kiuchumi na hivyo kuchochea maendeleo,” alisema.
Alisisitiza kuwa tovuti hii pia itasaidia kujenga mahusiano na mawasiliano kati ya warembo wa Miss Tanzania kwa upande mmoja  na wadau wa maendeleo ndani na nje ya nchi.
“Tutawashirikisha wadau mbalimbali katika swala hili muhimu na ni wito wetu kwamba wasituangushe kwa faida ya nchi yetu,” alisema Bw. Prashant.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa tovuti hiyo, Bw. Ali Zoeb aliwaahidi warembo walioshiriki uzinduzi huo kuwa tovuti hiyo itasaidia sana katika kuwaunganisha na wadau mbalimbali ndani na nje ya nchi na kuwasisitiza warembo popote walipo kuanza kujenga mazoea ya kutembelea tovuti hiyo na kujua kinachojiri.

Naye, mshauri wa habari wa tovuti hiyo, Bw. Peter Keasi alisema tovuti na jarida litakaloanzishwa hivi karibuni vitasaidia kurahisisha mawasiliano kufanya kazi kama daraja baina ya warembo hapa nchini, jambo alilosema ni muhimu kwa maendeleo.

Uzinduzi huo ulishuhudiwa na warembo walioko kwenye kambi ya Miss Tanzania kwa sasa pamoja na wadau wengine wa urembo hapa nchini.

Mwisho

Friday, October 26, 2012

NAIBU WAZIRI AELEZA KILICHOMFANYA KUSEMA TANZANIA NI MUUNGANIKO WA ZIMBABWE NA PEMBA



Naibu Waziri Philipho Mulugo
Kuanzia juzi taarifa na video ya Naibu Waziri wa Elimu na mafunzo ya ufundi wa Tanzania Philipo Augustino Mulugo zimeanza kusambaa kwa watanzania wengi kuhusu alichosema akiwa Afrika Kusini kwenye mkutano wa kimataifa  kwamba Tanzania ni muungano wa visiwa vya bahari ya Hindi, Pemba na Zimbabwe.

Mulugo leo amezungumza na Power Breakfast ya CLOUDS FM na kusema kabla ya yeye kupanda kuanza kuzungumza kulikua na kiongozi wa Zimbabwe ambae alitoka kuzungumza na nina mkariri akisema

 “sasa ilibidi lazima baada ya kufika pale ni lazima umshukuru mwenzako aliepita sasa kama mawazo ndiyo yaliyokua yamedhania hivyo kwamba basi hapa naitamka Zimbabwe kwa sababu zote zimeanzia na Z labda ilitokea hivyo lakini nakiri kabisa kwamba sikua na makusudio kwamba naitamka Zimbabwe lakini kule kwenye power presentation inaonekana kabisa ukifungua pale ni Tanzania imeungana na Zanzibar Pemba na Tanganyika kama ambavyo tunajua kwa sababu ile ni historia hakuna asiejua hata mtoto wa darasa la tatu”

“Niseme tu kwamba hiyo ni kuteleza kwa ulimi na nilikua namfikiria yule waziri wa Zimbabwe kwa sababu alikua ametoka kuhutubia kabla ya mimi, nilikua naomba ieleweke hivyo………… 

na wengi wameongea wanahoji lugha kiingereza, jamani tukubaliane kwamba kusema Zimbabwe badala ya Zanzibar sidhani kama inaendana na drama yenyewe kwa sababu mimi nimekua mwalimu mda mrefu nimefundisha wanafunzi wangu na wananifahamu uwezo wangu mkubwa na tena mimi ni mwalimu wa historia hata degree yangu ni mimi ni mwalimu wa historia na Economics, 

labda niliongea nilikua sijielewi na ningegundua nimetamka Zimbabwe ningeweza kuomba radhi, mataifa yote wawe waafrika wawe wazungu wengi huwa tunazingatia kuangalia kwenye power point pale, wengi huwa hawasikilizi sauti” – Mulugo

Kuhusu kukosea kutaja mwaka, Namkariri naibu waziri akisema “mimi pale nia yangu ilikua ni kusoma namba moja moja  nikashtukia nakwenda kusoma mbili, haijakaa kama nimekosea kiingereza kama watu wanavyoipanua kwa mfumo huo lakini kama watu wamenielewa hivyo niombe tu msamaha”(SOURCE djfetty.blogspot.com)

Thursday, October 25, 2012

UVCCM WAPUUZIA AGIZO LA JK





UVCCM WAPUUZA AGIZO LA JK

MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Jakaya Kikwete jana alifungua rasmi Mkutano Mkuu wa Jumuiya ya Vijana wa chama hicho (UVCCM), huku akiwaambia kwamba “watajuta”, ikiwa watachagua viongozi kwa misingi ya rushwa.
“Nawaambieni, mkifanya mchezo ipo siku mtakuja kujuta maana mkishamchagua kiongozi asiyefaa, mtalazimika kuwa naye huyohuyo hadi 2017, na kama Waswahili wanavyosema majuto ni mjukuu,” alisema Rais Kikwete.
Kauli hiyo ya Rais Kikwete ni kama aliyoitoa Jumapili usiku wakati akiahirisha mkutano mkuu wa Jumuiya ya Wanawake ya chama hicho (UWT) pale aliposema CCM kinakwenda kubaya kutokana na chaguzi zake kugubikwa na vitendo vya rushwa.
Katika hotuba yake hiyo ya Jumapili, Rais Kikwete alisema siku zilizopita vitendo hivyo vilikuwa vikihusishwa zaidi na wanaume, lakini akaeleza kushangazwa kwake na makundi ya kina mama nao kuanza kujihusisha na rushwa.
Hata hivyo, kauli hizo za Rais Kikwete zilianza kupuuzwa usiku wa kuamkia jana kutokana na madai ya kushamiri kwa vitendo hivyo vya rushwa miongoni mwa wajumbe.
Vitendo hivyo vya rushwa vinadaiwa kutolewa na makundi ya wanasiasa wanaotafuta kuungwa mkono ndani ya CCM katika kinyang’anyiro cha urais kwenye Uchaguzi Mkuu ujao wa 2015.
Waandishi wetu ambao walitembelea sehemu mbalimbali hasa hoteli na nyumba za kulala wageni kati ya saa nne usiku na tisa alfajiri, walishuhudia harakati za kutoa na kupokea fedha ili kushawishi wajumbe kuwapigia kura wagombea wanaowataka.
Usiku wa saa 7:30, mmoja wa makada wa CCM alimwambia mwandishi wetu kwamba kuna fedha nyingi zimemwagwa katika uchaguzi huo na kwamba hata vyombo vya usalama kama Polisi, Usalama wa Taifa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), ni kama havipo.
“Kama hata ninyi waandishi wa habari mnashindwa kuandika haya tunayoyaona usiku huu, basi nchi hii inakwenda pabaya sana. Maana nyie ndiyo mliobaki na hakuna mtetezi wetu mwingine. Chama chetu kimekuwa cha ajabu sana, hakuna jinsi unaweza kupata uongozi bila fedha,” alisema.
Baadhi ya wajumbe walidai kwamba kulikuwa na gari ambalo lilikuwa likizunguka na kiasi kikubwa cha fedha ambazo zilikuwa zikigawanywa kwa wajumbe katika hoteli na nyumba za kulala wageni walikofikia.
Katika kufuatiliana, takriban saa 8.30 usiku, magari ya kambi tofauti yalionekana yakikimbizana katika eneo la Area ‘C’, baada ya wajumbe wa kambi moja kuwahisi wenzao kwamba walikuwa wakigawa fedha hivyo kutaka kuwakamata.
Ulikuwa ni kama mchezo wa kuigiza kwani wakati mwingine, magari yalikuwa yakikutana katika makazi ya wajumbe na ilipotokea hivyo yote yalisita kusimama na badala yake yaliendelea na safari na baadaye kurejea.
Kulikuwa na taarifa kwamba wajumbe wa mkutano huo kutoka Tanzania Zanzibar walihamishwa kwa muda usiku baada ya kupewa fedha na kambi mojawapo, kwa lengo la kuhofia kwamba kambi nyingine ingewabadilisha mawazo.
Mkakati pia unadaiwa kusukwa kuwahamisha wajumbe wa Mikoa ya Mbeya na Singida kwa nyakati tofauti, lakini jaribio hilo liligonga mwamba kutokana na wajumbe hao kukataa kwamba ulikuwa ni usumbufu kutokana na kuchoka kwa safari ndefu.
Katika moja ya hoteli zilizopo Area ‘C’, mwandishi wetu alishuhudia baadhi ya wajumbe kutoka mikoa kadhaa wakiingia hotelini hapo saa 7:15 usiku na baada ya dakika kama 10 hivi, waliingizwa kwenye chumba maalumu ambako walikaa kwa zaidi ya saa nzima.
Saa 7:54 usiku, umeme ulikatika Mji mzima wa Dodoma na ulirejeshwa saa 8.08, tukio ambalo baadhi ya wajumbe walidai kwamba huenda ulikuwa mpango wa kufanikisha kugawa fedha katika baadhi ya maeneo yaliyokuwa yakihofiwa kutokuwa na usalama.
Uchaguzi wa UVCCM kwa ujumla wake umevuta makada wengi wa chama hicho wakiwamo mawaziri na wabunge ambao walikuwa washiriki rasmi wa kampeni hizo za usiku wa kuamkia jana.

Kauli ya Kikwete
Rais Kikwete wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Nane wa UVCCM jana, alikiri kuwa mwelekeo wa CCM si mzuri hivyo akawaomba vijana “kukinusuru chama chao”.
Alisema watu wamekuwa wakikisema vibaya jambo linalomfanya aone kuwa umefika wakati ya kuwapo mabadiliko.
“Chama chetu kinasemwa vibaya kila mahali kwamba sisi lazima mtu aununue uongozi kwa fedha na kwamba kura zinanunuliwa, hivi jamani sisi tunakwenda wapi, vijana lazima mbadilike,” alisema Kikwete na kuongeza:
“Nayasema haya kwa dhati ya moyoni kuwa ni lazima tubadilike na umefika wakati sasa ambao kila mmoja wetu afanye mabadiliko na mabadiliko lazima yaanzie kwenu vijana.”
Rais aliwaagiza vijana kutumia Ibara ya Tano ya Katiba yao ambayo inaelekeza kuwa nia ya CCM ni kuhakikisha kuwa chama kinabaki madarakani wakati wote bila ya kuyumba.
Alisema kuwa vijana hao wakijipanga wanaweza kukisaidia CCM kuendelea kubaki madarakani kizazi hadi kizazi na nchi wakati wote itakuwa chini ya chama hicho.
Alisema CCM si chama cha michezo, kama mpira wa miguu, bali ni chama cha siasa ambacho kinapaswa kuwa makini wakati wote.
Awali, akimkaribisha Rais Kikwete, Kaimu Mwenyekiti wa UVCCM, Benno Malisa alikiri kuwa wakati mwingine vijana walikuwa wakikimbia mwendo mrefu kiasi cha kukwazana na chama.
Malisa alimpongeza Rais Kikwete kwa kuwa mvumilivu katika yote akisema kama angeamua kusimama katika haki, ni wazi kuwa hata yeye (Malisa) asingekuwa katika nafsi hiyo.
Mwenyekiti huo alijivunia mafanikio kuwa amemaliza kuongoza umoja huo akiacha ujenzi wa jengo la kitega uchumi la ghorofa 16.

Ushindani mkubwa
Makundi ya vijana yalianza kujikusanya nje ya Ukumbi wa Chuo cha Mipango Dodoma jana saa mbili asubuhi, huku yale yaliyokuwa yakiwaunga mkono baadhi ya wagombea yakiimba nyimbo za hamasa yakiwa yamebeba picha za wagombea husika.
Wakati huo ulinzi uliimarishwa kwani gari la Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) likiwa na askari wapatao 12 lilikuwa likizunguka eneo hilo na baadaye kuegeshwa mbele ya ukumbi huo.
Kazi kubwa ilikuwa ni ya kugawa mamia ya vipeperushi vyenye wasifu wa wagombea wa nafasi mbalimbali za uongozi, ambayo kwa kiasi kikubwa ilifanywa na wapambe wa wagombea husika wakisaidiwa na baadhi ya makada wa CCM wa mjini Dodoma.
Mmoja wa makada hao (jina tunalihifadhi kwa sasa) alisema kazi hiyo ilikuwa ikifanywa kwa ujira kati ya Sh10,000 na 20,000.
Vita kubwa katika uchaguzi huo ni katika nafasi ya Makamu Mwenyekiti iliyokuwa ikiwaniwa na Paul Makonda, Mboni Mhita na Ally Salum Hapi, wakati nafasi ya Mwenyekiti ni Sadifa Juma Khamis, Rashid Simai Msaraka na Lulu Msham Abdallah.
Hadi tunakwenda mitamboni jana jioni, Sadifa Juma Khamis alishinda nafasi ya Uenyekiti wakati kwa upande wa Makamu Mwenyekiti Mboni Mhita alikosa kura 30 kufika nusu ya kura zote zilizopigwa na Paul Makonda alishika nafasi ya pili.
Kutokana na matokeo hayo, uchaguzi wa nafasi ya Makamu Mwenyekiti Taifa ilibidi urudiwe ili kupata mshindi kwa nusu ya kura zote. (source mwananchi.com)


KENYATTA AOMBA MSAADA WA KIKWETE URAISI KENYA



KESI inayowakabili Wakenya wanne kuhusu vurugu za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2008 iliyopo katika Mahakama ya Kimataifa ya Makosa ya Uhalifu wa Kivita (ICC), imechukua sura mpya baada ya mmoja wa watuhumiwa hao, Uhuru Kenyatta kwenda na ujumbe wake kwa Rais Jakaya Kikwete kumwomba amuunge mkono katika harakati zake za urais.
Kwa mujibu wa gazeti la Standard la Kenya, Rais Kikwete alikutana na kiongozi huyo wa Chama cha The National Alliance Ikulu na kufanya naye mazungumzo yaliyodumu kwa saa tatu.
Katika kikao hicho pia kulikuwa na wajumbe wengine kutoka chama cha URP cha William Ruto na wale wa New Ford Kenya wakiongozwa na Waziri wa Sheria, Eugine Wamalwa anayetajwa kuwa mgombea mwenza wake. 
“Kenyatta alisema kuwa malengo yake na viongozi wenzake ni kuipeleka Kenya mbele wakiwa na umoja. Kwa kumalizia akasema, wanalenga kuwafikia viongozi wa vyama vya siasa,” alisema Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Kenyatta, Munyori Buku.
Ujumbe wa Uhuru umekuja ikiwa ni siku moja kabla ya kuwasili Nairobi kwa Mwendesha Mashtaka Mkuu wa  ICC, Fatou Bensouda kwa ajili ya mazungumzo na viongozi wa nchi hiyo na kujionea maeneo yaliyoathiriwa na vurugu hizo. 
Umuhimu wa safari hiyo pia umetokana na safari ya Katibu Mkuu mstaafu wa Umoja wa Mataifa, Kofi Annan na Rais mstaafu wa Tanzania, Benjamin Mkapa nchini Kenya hivi karibuni, huku wakiwa na ujumbe kwamba Kenyatta na Ruto hawana sifa mbele ya Wakenya na jumuiya ya kimataifa ya kugombea urais.
Annan ndiye aliyesimamia mchakato wa amani katika kazi ambayo alisaidiana na Rais Kikwete na Mkapa.
Annan na Mkapa inasemekana walikwenda Nairobi na kufanya majadiliano na Rais Mwai Kibaki yanayoaminika kujikita katika kesi hiyo ya ICC sanjari na Uchaguzi Mkuu wa Machi 4, 2013.
Inaaminika kuwa ujumbe huo kutoka Kenya ulikuja makusudi kwa Rais Kikwete hasa kwa kuwa ana uhusiano mzuri na viongozi wakubwa wa mataifa ya Magharibi akiwa pia amechangia katika kuleta amani nchini humo baada ya vurugu za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2008.
Hivyo wamelenga kumtuma Rais Kikwete kupeleka ujumbe ICC ili kuwaruhusu wagombee katika Uchaguzi Mkuu kwa manufaa ya uchaguzi wa amani na Kenya kwa jumla. 
Katika ziara yake, Annan alikaririwa akisema: “Ni kweli kuna mambo ambayo kila mtu angependa yaangaliwe hasa kwa watu wanaotajwa kugombea urais.”
Kauli hiyo imewatisha Uhuru na Ruto ambao walilipuka wakimtaka Annan kuachana na mambo ya Kenya.
Kuhusu hilo Buku alisema: “Wakenya ndiyo waamuzi wa hatima yao … Rais Kikwete ameombwa kushawishi kuheshimiwa kwa uamuzi wa Wakenya. Ndiyo waamuzi wa hatima yao hivyo ni lazima waruhusiwe kuchagua viongozi wao bila kuingiliwa. Rais amegusia kwamba, Afrika ingeheshimu uamuzi, Wakenya wangefanikisha uchaguzi mkuu wa Machi mwakani.
“Hatuna matatizo na marafiki zetu, lakini kama hawatuheshimu hilo ni shauri yao, tuna marafiki wengi wa kufanya nao kazi ulimwenguni kote,” alisema Uhuru wiki iliyopita jijini Nairobi.
Akiwa nchini, inasemekana kuwa Uhuru alikuwa akirudia maoni yake kwa Rais Kikwete kwamba ni makosa kwa wageni kuingilia uchaguzi wa Kenya. 
Katika hatua nyingine, mwandishi wa Mwananchi alimshuhudia Kenyatta akiwa katika Mgahawa wa Rose Garden, Dar es Salaam akipata vinywaji na nyama choma.
Baada ya kuingia Rose Garden akiongozana na Balozi wa Kenya nchini Tanzania, Mutinda Mutiso, wateja na watu mbalimbali walikwenda kumsalimia mtoto huyo wa Rais wa Kwanza wa Kenya, Jomo Kenyatta ambaye alionekana mwenye furaha na hakukuwa na ulinzi mkubwa.(SOURCE mwananchi.com)